ACT WAZALENDO WAICHACHAMALIA SERIKALI YA MAGUFULI,YAIKABA KOO TENA ,SOMA HAPO KUJUA
CHAMA Cha ACT-Wazalendo sasa kinataka serikali
imwelekeze Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kufanya ukaguzi
maalum kwenye utoaji wa vibali vya kuuza chakula nje mwaka jana, anaandika
Pendo Omary.
Uongozi
wa chama hicho umekuja na rai hiyo katika kukazia hoja ya kiongozi wao mkuu,
Zitto Kabwe ya kuweka rehani ubunge wake iwapo atathibitishiwa na serikali kwa
kuona mwenyewe kuwepo kwa tani 1.5 milioni za chakula kwenye maghala ya akiba
yanayosimamiwa na Wakala wa Chakula cha Akiba nchini (NFRA).
Leo Ado Shaibu, Katibu wa Kamati ya Itikadi,
Mawasiliano ya Umma na Uenezi wa ACT Wazalendo ametoa taarifa ya maandishi
ikisema kuwa hoja ya chama inasimamia takwimu rasmi za serikali zilizotolewa
katika njia mbalimbali mwaka jana.
Shaibu amesema serikali inaposema kwamba imeelekeza
kuanza kusambazwa chakula kipatacho tani milioni 1.5 zilizopo kwenye maghala
yake ya akiba, inaonesha kuna kitu hakisemwi kwa ukamilifu wake.
Amesema Zitto anaposhikilia hoja ya kuweka rehani
ubunge wake anazingatia takwimu rasmi zilizotolewa na serikali kupitia vyombo
vyake. Kwa mujibu wa taarifa ya serikali, kufikia mwezi Oktoba mwaka jana
kulikuwa na akiba ya chakula tani 90,476 kwenye maghala yake.
Maeneo yote yanayotajwa kuwa na tishio la
njaa,ukweli ni kwamba chakula pekee ambacho serikali inakimiliki na ina uwezo
wa kukisambaza ni kile kilicho NFRA, ambacho mpaka mwezi Oktoba kulikuwa ni
tani 90,476 tu.
Akinukuu taarifa ya Wizara ya Fedha na Mipango ya
mwezi Juni mwaka jana kuhusu Hali ya Uchumi wa Taifa, Shaibu amesema uzalishaji
wa mahindi kwa msimu uliopita, ulipungua kwa asilimia 12.3 wakati uzalishaji wa
ngano na mtama/uwele ulipungua kwa asilimia 57 na asilimia 19 kwa mfuatano huo.
“Serikali inatoa wapi hizo tani milioni 1.5? Je,
inaahidi kusambaza chakula hewa?,” amehoji Shaibu katika hoja ya ACT-Wazalendo
inayolalia taarifa zinazohusu mavuno ya msimu uliopita.
Shaibu amesema mchele tu ndio uzalishaji wake
uliongezeka kwa asilimia 15, ndiyo maana “Serikali ilitoa vibali vya kuuza
mchele nje baada ya kuwa soko la ndani limejaa mchele kutoka Pakistan na
kadhalika.”
Anasisitiza kwamba kwa kuongezea vibali
vilivyotolewa na serikali vya kuuza mahindi (au unga wa mahindi) nje, “utaona
kuwa kuna kila sababu ya kutaka ukaguzi maalumu wa mdhibiti kwenye mchakato wa
utoaji wa vibali vya kuuza nafaka nje ya nchi.”
Amesema “Tunaiomba ofisi ya CAG ifanye ukaguzi
maalumu kukagua vibali vya kuuzwa chakula nje mwaka jana ili kujua ukweli wa
jambo hili. Likithibitika kuwa ni kweli ni wazi kuwa serikali itabidi iwajibike
kwa kuweka mbele maslahi ya kibiashara badala ya maslahi ya maisha ya wananchi.”
Jana Zitto ambaye ni mbunge wa Kigoma Mjini
alitangaza kuweka rehani ubunge wake iwapo kutakuwa na uthibitisho wa serikali
kumiliki chakula cha akiba kipatacho tani 1.5 milioni. Tamko lake lilikuja
baada ya Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu kutangaza kwamba serikali itaanza
kusambaza chakula kwenye maeneo yenye uhaba huku akipinga taarifa kupitia
vyombo vya habari kwamba kuna balaa la njaa nchini.
Waziri Mkuu Majaliwa aliyekuwa katika uzinduzi wa
safari za ndege za ATCL kati ya Dodoma na Dar es Salaam, aliongeza shutuma kwa
vyombo vya habari kutumika na baadhi ya wafanyabiashara kueneza taarifa
alizosema si sahihi na zinatolewa kwa maslahi ya wafanyabiashara wanaoingiza
chakula nchini.
Msimamo huo unatokana na kauli ya Rais John Magufuli
kutangaza kwamba hakuna uhaba wa chakula wala njaa popote nchini na kwamba hata
wale wenye shida ya chakula kutokana na ukame katika msimu huu wasitarajie
kupewa chakula bure na serikali.