Zinazobamba

CHADEMA YAKUTANA 'CHOBINGO',SOMA HAPO KUJUA

Kamati Kuu ya Chadema wakishikana mikono kuonyesha mshikamano
KAMATI Kuu (CC) ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), inaanza kikao chake leo, ambacho pamoja na mambo mengine kitajadili hali ya kiuchumi na kisiasa ya nchi, anaandika Charles William.
Tumaini Makene, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Chadema amesema kuwa kikao hicho kinakaa kwa siku mbili jijini Dar es Salaam siku ya leo na kesho (Oktoba 22 na 23).
“Pamoja na mambo mengineyo lakini pia Kamati Kuu itapokea na kujadili kwa kina hali ya kisiasa hapa nchini na kupitisha mazimio kadhaa,” amesema.


Katika kikao hicho cha siku mbili huenda Chadema ikaibuka na mipango mipya ya kujiimarisha katika kipindi hiki ambacho mikutano ya hadhara ya viongozi wa vyama vya siasa imepigwa marufuku na Rais John Magufuli.
Itakumbukwa kuwa kikao cha dharura cha CC ya Chadema kilichokaa mwezi Julai mwaka huu kiliibuka na azimio la kufanya mikutano ya maandamano na mikutano ya hadhara nchi nzima chini ya mwamvuli wa Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania (Ukuta).
Hata hivyo chama hicho kiliahirisha mpango wake huo uliopangwa kufanyika tarehe 1 Septemba, kwa madai kuwa kiliombwa na viongozi wa dini kabla ya kutangaza kuachana na mpango huo rasmi mnamo Septemba 30 mwaka huu na kuahidi kuibuka na mbinu mpya.